Alhamisi 12 Februari 2026 - 16:30
Jamhuri ya Kiislamu haitaafikiana juu ya haki yake ya kupata na kutumia teknolojia ya nyuklia ya amani

Hawza/ Balozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran nchini Lebanon alisema: katika njia ya maendeleo, Jamhuri ya Kiislamu kamwe haitapuuzia haki yake halali na isiyoweza kujadiliwa ya kupata na kutumia teknolojia ya nyuklia ya amani.

Kwa mujibu wa ripoti ya kitengo cha tarjama cha Shirika la Habari la Hawza, Mojtaba Amani, balozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran nchini Lebanon, kutokana na mnasaba wa maadhimisho ya miaka arobaini na saba ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran, aliandaa hafla rasmi katika Hoteli ya Phoenicia, Beirut.

Katika hafla hiyo, walihudhuria wawakilishi wa Rais, Spika wa Bunge na Waziri Mkuu wa Lebanon, mawaziri, mabalozi wa nchi za kigeni, pamoja na shakhsia za kisiasa, kijeshi, kidini, kijamii na vyombo vya habari. Miongoni mwa waliokuwepo ni mwakilishi wa Nawaf Salam (Waziri Mkuu), mwakilishi wa Joseph Aoun (Rais), Waziri wa Afya Rakan Nasseraldin, mwakilishi wa Spika wa Bunge Nabih Berri, mwakilishi wa Waziri wa Mambo ya Nje Rola Noureddine, Moussa Karneib (mwakilishi wa Waziri wa Mambo ya Ndani Ahmad al-Hajjar), na wabunge Ghazi Zeaiter, Hassan Fadlallah, Mohammad Raad, Hussein al-Hajj Hassan, Ali Fayad, Tony Frangieh (akiwakilishwa na Jean Boutros), Haidar Nasser, Gebran Bassil (akiwakilishwa na Mansour Fadel), pamoja na shakhsia nyengine.

Pia Sheikh Hassan Abdullah alihudhuria kwa niaba ya Sheikh Ali al-Khatib, Naibu Mkuu wa Baraza Kuu la Kiislamu la Mashia wa Lebanon, na Najji Saab kwa niaba ya Sheikh Aql wa Duruzi, Sami Aboul-Mona.

Hafla ilianza kwa kusomwa aya za Qur’ani Tukufu, kisha zikapigwa nyimbo za taifa za Lebanon na Iran, na baadaye filamu ya kumbukumbu kuhusu mafanikio ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ikaonyeshwa.

Iran imethibitisha kuwa katika kila mlinganyo wa kimataifa ni nguvu isiyoweza kupuuzwa

Akiendelea, Balozi Amani alisema: Kutoka Beirut pendwa, mji wa asili na wa fahari, katika msimu wa maadhimisho ya miaka 47 ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu, yaliyoongozwa na Imam Khomeini (q.s), ninawakaribisha nyote. Mapinduzi hayo yalikuwa mapinduzi ya wanyonge na watu huru, yaliyoibadilisha historia ya Iran, yakatikisa viti vya enzi vya madhalimu, yakarejesha heshima ya mwanadamu, na kuhuisha matumaini katika nyoyo za mataifa yaliyodhulumiwa ili kurejesha uhuru, kujitegemea na maisha ya heshima.

Aliongeza kuwa; tangu siku hiyo ya kihistoria, dunia imeshuhudia mabadiliko makubwa ya kijiografia ya kisiasa; falme zilianguka, mikataba ikabadilika, nadharia na miradi ya kisiasa ikaanguka, lakini mti wa Mapinduzi ya Kiislamu ukatia mizizi ardhini na matawi yake yakapaa juu. Katika miongo hii, dunia ilitoka mfumo wa pande mbili kwenda upande mmoja, na hatimaye kufikia hali ya sasa ambamo enzi ya utawala wa mabavu imefikia mwisho na zama za nguvu huru, zikiongozwa na Iran yenye nguvu, zimeanza — Iran ambayo imethibitisha kuwa katika kila mlinganyo wa kimataifa ni nguvu isiyoweza kuondolewa.

Tulibadili vikwazo vya kidhalimu kuwa fursa ya kustawi kwa uchumi wa kujitegemea

Akimzungumzia maendeleo ya ndani, alisema: Taifa la Iran limejitahidi kutekeleza misingi na malengo ya mapinduzi, ikiwemo kuimarisha utawala wa sheria na uhuru. Haya yameambatana na maendeleo ya kisayansi, kiuchumi, kijeshi na kiteknolojia. Leo Iran imefika anga za juu, inaongoza katika teknolojia ya nano na seli shina, na vyuo vikuu vyake vimo katika viwango vya juu duniani.

Aliendelea kusema: Tulibadili vikwazo vya kidhalimu kuwa fursa ya kustawisha uchumi wa kujitegemea, tukafikia kujitosheleza katika bidhaa za kimkakati na kukuza viwanda vya kitaifa. Leo Iran inaathiriwa kidogo zaidi na misukosuko ya masoko ya kimataifa, hadi silaha ya vikwazo imepoteza ufanisi wake na kuwa mzigo kwa walioviweka.

Amani alisisitiza: Katika njia ya maendeleo, Jamhuri ya Kiislamu haitawahi kuachana na haki yake halali na isiyoweza kujadiliwa ya kupata na kutumia teknolojia ya nyuklia ya amani. Tunachukulia haki hii kuwa nguzo ya mamlaka ya kitaifa na maendeleo ya kiuchumi, na hakuna tishio wala vikwazo vitakavyotuzuia kuendelea na njia hii ya kisayansi na ustaarabu.

Tunaiona nguvu ya Lebanon, jeshi lake na muqawama wake kuwa dhamana ya utulivu wa eneo lote

Balozi wa Iran aliongeza kuwa: Chini ya miongozo ya Kiongozi Mkuu wa Mapinduzi, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imejenga sera ya kigeni yenye uwiano juu ya ujirani mwema, kuheshimiana na ushirikiano wa kujenga katika eneo. Iran imekuwa ikionya daima juu ya hatari ya utawala wa Kizayuni katika eneo — utawala ambao ni tishio kwa Palestina, usalama wa Kiislamu, Kikristo na Kiarabu wa eneo, pamoja na ardhi na rasilimali za mataifa yake.

Alisisitiza kuwa: Kuitetea nguvu ya Lebanon na muqawama wake tukufu, uliovunja dhana ya ubora wa Kizayuni, ni kuutetea umoja, heshima na ukamilifu wa ardhi ya nchi hii. Kujitoa muhanga watu wa Lebanon kumezuia ndoto ya upanuzi wa Israel. Tunaona nguvu ya Lebanon, jeshi lake na muqawama wake kuwa dhamana ya utulivu wa eneo lote, na mikutano ya mara kwa mara ya viongozi wa Iran na Lebanon ni ushahidi kwamba tuko katika handaki moja dhidi ya tamaa za maadui.

Maadui wamekata tamaa ya mapambano ya kijeshi dhidi ya Iran

Aliendelea kusema: Iran inaamini katika kuendeleza uhusiano na Lebanon kwa manufaa ya mataifa yote mawili, na inashirikiana na makundi yote ya kidini, kimadhehebu na kisiasa ya Lebanon. Iran pia inaunga mkono juhudi za kusimamisha mashambulizi ya Israel, kumaliza ukaliaji wa ardhi, kuwaachia wafungwa na kuijenga upya Lebanon.

Balozi Amani alisema: Maadui waliokata tamaa ya mapambano ya kijeshi dhidi ya taifa la Iran hivi karibuni walijaribu kutumia vibaya maandamano ya kitaaluma nchini Iran ili kusababisha machafuko. Uchochezi wa vyombo vya habari na ufadhili wa kigeni ulidhihirisha chuki ya kipofu dhidi ya Iran. Lakini taifa la Iran linatofautisha wazi kati ya maandamano halali na utegemezi kwa mipango ya wageni. Mamilioni ya Wairani walijitokeza katika maandamano ya hiari kuonesha upya utii wao kwa mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu, wakithibitisha kuwa mti wa mapinduzi ni imara zaidi kuliko kuyumbishwa na fitna.

Marekani inajua vizuri kuwa zama za “piga ukimbie” zimepita

Mwisho, alisema: Mapambano kati ya Iran na tawala mbalimbali za Marekani tangu mwanzo wa mapinduzi ni mapambano kati ya roho mbili: roho ya uonevu na utawala wa mabavu dhidi ya roho ya uhuru na uadilifu. Leo imekuwa wazi kwamba Marekani, licha ya kudai kutetea haki za binadamu, ndiyo mvunjaji mkubwa wa haki hizo, kwa sababu inaunga mkono bila masharti vita na uhalifu wa Wazayuni. Marekani inajua vyema kuwa zama za “piga ukimbie” zimekwisha, na jaribio lolote la kijeshi dhidi ya Iran litajibiwa kwa jibu kali, la haraka na la kuumiza popote.

Katika hitimisho la hotuba yake, Balozi Amani alisema: “Niruhusuni nihitimishe kwa neno kutoka moyoni. Wakati nimesimama kati yenu leo, muda wa jukumu langu la kidiplomasia katika nchi hii pendwa unakaribia mwisho. Baada ya siku chache nitaondoka Lebanon kimwili, lakini moyo wangu utabaki katika mitaa ya Beirut, fahari ya milima ya kusini na wema wa watu wa Bekaa, Jabal na kaskazini.”

Aliendelea kusema: “Ilikuwa heshima kwangu kuiwakilisha nchi yangu katika ardhi hii kubwa na kushuhudia ukarimu, azma thabiti na uwezo wa watu wa Lebanon wa kuvuka matatizo kwa tabasamu na subira. Mwisho wa jukumu langu rasmi si mwisho wa uhusiano wangu na watu wa nchi hii ninayoipenda; kwani yeyote anayeishi Lebanon hata kwa siku moja, Lebanon hubaki ndani yake milele. Ishi Lebanon, nchi huru, yenye fahari na muqawama; na ishi Iran, taa ya heshima na utu. Rehema na milele kwa mashahidi wetu watukufu.”

Lebo

Maoni yako

You are replying to: .
captcha